WANAWAKE KENYA KUPATIWA MAPUMZIKO WANAPOKUWA KWENYE HEDHI

Serikali ya Kaunti ya Nairobi nchini Kenya imeidhinisha rasmi utaratibu wa kutoa siku mbili kila mwezi za kupumzika kwa sababu ya hedhi kwa wanawake wafanyakazi, kama sehemu ya mfumo wa rasilimali watu wa kaunti hiyo.

Uamuzi huu umefikiwa baada ya kikao cha baraza la mawaziri kilichoongozwa na Gavana wa jimbo hilo Johnson Sakaja, kilichopendekeza kuingiza usaidizi wa afya ya hedhi katika sera za rasilimali watu, kwa lengo la kuboresha ustawi wa wafanyakazi na kuongeza utendakazi wawanawake kazini.

Taarifa ya kaunti inabainisha kuwa changamoto za afya ya hedhi, hususan dysmenorrhea (maumivu makali ya hedhi), huathiri kwa kiasi kikubwa ustawi wa wanawake na utendaji wao kazini.

Tafiti zinaonyesha kuwa kati ya wanawake 65 hadi 80 kwa mia hukabiliwa na maumivu ya hedhi, na idadi kubwa ufanisi wao kazini huathirika zaidi.

Kwa kuwa wanawake wanajumlisha zaidi ya nusu ya wafanyakazi wa Kaunti ya Nairobi, changamoto hizi zinachangia kupungua kwa ufanisi, kuwepo kazini licha ya ugumu wa kiafya (presenteeism) na kuathiri huduma za umma.

Hadi sasa, afya ya hedhi haikuwa imeingizwa katika sera za rasilimali watu, jambo lililowalazimisha wanawake kwenda kazini wakiwa wagonjwa.

Sera mpya itawaruhusu wanawake kusitisha kazi kwa siku mbili kila mwezi bila kuongeza mzigo wa kifedha kwa kaunti, na hivyo kutoa msaada wa kimuundo kwa wafanyakazi.

Kulingana na waraka wa baraza la mawaziri, sera hii imejengwa kwa msingi wa ushahidi na inalingana na ahadi za kaunti za usawa wa kijinsia, kazi yenye heshima na utawala jumuishi.

Nchi nyingine zilizo na haki za likizo ya hedhi ni pamoja na Zambia, Japan na Korea Kusini-ambapo Sheria ya Viwango vya Kazi inawataka waajiri kutoa siku moja ya likizo ya hedhi kwa mwezi.

Indonesia hutoa siku mbili za kisheria, zilizochukuliwa siku ya kwanza na ya pili ya hedhi wakati maumivu yanaripotiwa, wakati Uhispania ilianzisha sheria sawa mnamo 2023

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *